Breaking News

PROF MKENDA: AZINDUA TUZO YA TAIFA YA MWALIMU NYERERE

Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda akifafanua jambo katika hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu iliyofanyika leo Septemba 12, 2022 katika ofisi za Makao Makuu ya Benki ya CRDB jijini Dar es Salaam

Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda akizindua Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu leo Septemba 12, 2022 katika ofisi za Makao Makuu ya Benki ya CRDB jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Tanzania Dkt. Aneth Komba akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu iliyofanyika leo Septemba 12, 2022 katika ofisi za Makao Makuu ya Benki ya CRDB jijini Dar es Salaam
Mwenyekiti Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu Prof. Penina Mrama akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu iliyofanyika leo Septemba 12, 2022 katika ofisi za Makao Makuu ya Benki ya CRDB jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wadau wa Elimu nchini wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu iliyofanyika leo Septemba 12,2022 katika ofisi za Makao Makuu ya Benki ya CRDB jijini Dar es Salaam.

Dar es salaam:
WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema kwamba Serikali imetenga shilingi bilioni moja kwa mwaka huu wa fedha ili kuchochea ukuaji wa Sekta ya Vitabu nchini.

Prof. Mkenda amebainisha hayo leo jijini Dar es Salaam akizungumza katika hafla ya Uzinduzi wa Tuzo ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu ambayo mshindi atatangazwa Aprili 13, 2023 siku ambayo ni kumbukumbu ya kuzaliwa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Waziri Mkenda amesema hali ya uchapaji na usambazaji wa vitabu vya ziada vyenye ithibati nchini si ya kuridhisha hivyo Serikali imeamua kwamba itasimamia uchapishaji, kuvinunua na kuvisambaza mashuleni hadi Maktaba ya Taifa vitabu vya mshindi wa tuzo hiyo.

Amebainisha kwamba kupitia tuzo hiyo Serikali inafungua ukurasa wa kuchochea hari mpya katika uchapishaji na usomaji wa vitabu nchini pamoja na kuchangamsha soko la vitabu nchini.

“Tumetenga kwenye bajeti kiasi cha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuhakikisha tunaanzia kutekeleza mapendekezo ya wadau wetu na taratibu zote zitafanyika chini ya TET lengo ni kukidhi matakwa ya wadau kuchangamsha soko siyo kushuhudia baadhi ya taasisi za uchapashaji zinafungwa,” amesema Prof. Mkenda na kuongeza kuwa,

“Lakini pia ili watu wasome lazima wajue vilivyomo ndani na tunataka tutumie utaratibu huu kukuza Kiswahili ndiyo maana uandishi utatumia Kiswahili tutaanza na uandishi wa Riwaya na Mashairi baadaye tutakuja na Tamthilia na Hadithi fupi fupi,”.

Kwa upande wake Kamishna Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Lyabwene Mtahabwa amewasisitiza Waandishi wa vitabu kuandika kuhusu watoto kwani wamekuwa wakipitia changamoto ya mazingira magumu kwa kufanyiwa vitendo viovu ndani ya Jamii na wahusika ni ndugu zao wa karibu vitendo hivyo ni pamoja na kulawitiwa kubakwa, kupigwa, kunyanyapaliwa hivyo wakiandika vitabu itasaidia kubadilisha Jamii.

“Watoto ni tunu kubwa tuliyopewa na Mwenyezi Mungu kuwa baraka lakini Leo tukiwaangalia baadhi ya watoto wanavyoteseka kutokana na changamoto wanazokutana nazo machozi yananitoka kila nikisoma magazeti visa na mikasa yao ni vya kutisha kalamu yenu itawaokoa”. Amesema Prof. Mtahabwa.

Naye Mwenyekiti Tuzo ya Taifa Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu Bi.Penina Mrama amesema Mbunifu atakayeshiriki atatakiwa kuandika nyanja moja tu kwa mada atakayoichagua yaani riwaya au ushairi na andiko liwe makini litakalojikita katika masuala ya kijamii na dirisha ya kuwasilisha kutakuwa wazi kuanzia Septemba 13- Novemba 30 mwaka huu.

Aidha amesema majaji watapitia maandiko ya kila mshiriki atakayetuma kupitia barua pepe na Zawadi nono Kwa washindi itakuwepo ambapo mshindi wa kwanza atapewa kiasi cha shilingi milioni 10 huku wa pili akipatiwa shilingi milioni 7 na watatu atapewa milioni 5 hivyo Waandishi wote wa vitabu andikeni kazi nzuri na hii itakuwa kila mwaka .

Hata hivyo Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) Dkt. Aneth Komba amempongeza Pro. Makenda kwa ubunifu wake wa kuanzisha Tuzo hiyo yenye lengo la kukuza Sekta ya Uandishi na kuongeza ari ya kujisomea.

Ameahidi kuwa watahakikisha wanasimamia Tuzo hiyo kwa ili kufikia malengo makubwa yaliyokusudiwa.