Breaking News

RC CHALAMILA AZINDUA PROGRAM YA “KONEKT UMEME, PIKA KWA UMEME” JIJINI DAR

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, leo Oktoba 9, 2025, amezindua rasmi programu ya Konekt Umeme, Pika kwa Umeme iliyobuniwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) katika viwanja vya Mwembe Yanga, Wilaya ya Temeke.

Programu hiyo imeelezwa kuwa ni ya gharama nafuu, yenye ufanisi mkubwa, na inayotumia kiasi kidogo cha umeme ukilinganisha na nishati nyingine za kupikia.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mhe. Chalamila ameipongeza Wizara ya Nishati, TANESCO na wadau wa maendeleo kwa kuanzisha wazo hilo bunifu linalolenga kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kwa Watanzania.

> “Mpango huu ni mwanzo wa zama mpya katika historia ya huduma za umeme nchini. Unaunga mkono juhudi za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kukuza matumizi ya nishati safi,” alisema Chalamila.



Ameongeza kuwa matumizi ya nishati safi ya umeme katika kupikia yatachangia kuboresha viwango vya maisha ya Watanzania na kuimarisha uchumi wa nchi.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, alisema Tanzania kupitia Wizara ya Nishati na TANESCO imetangaza mpango wa kitaifa wa nishati (Energy Compact) wenye lengo la kuunganisha wateja milioni 8.5 ifikapo mwaka 2030, sawa na wateja wapya milioni 1.7 kila mwaka.

Bw. Twange alibainisha kuwa programu ya Konekt Umeme, Pika kwa Umeme imezinduliwa katika kipindi sahihi, kwani inatoa fursa kwa wateja kupewa majiko ya umeme wakati wa kuunganishiwa huduma, na kulipa kidogo kidogo kupitia mfumo wa token.

“Mpango huu utasaidia familia nyingi kupika kwa ufanisi na kwa gharama nafuu,” alisisitiza Twange.

Mwisho wa hafla hiyo, Mhe. Chalamila aligawa majiko ya nishati safi ya umeme kwa wananchi mbalimbali na kuwataka wawe mabalozi wa matumizi ya nishati safi katika jamii zao.