Breaking News

NJIA YA KUSAFIRISHA UMEME KUTOKA BWAWA LA JULIUS NYERERE YA CHALINZE - DODOMA IMEKAMILIKA - MRAMBA

# Umeme wa JNHPP kufika Dodoma kupitia Chalinze

# SGR kupata njia yake maalum ya umeme, kuimarisha uhakika wa huduma

Dodoma - Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi Mramba, amesema Njia ya Kusafirisha Umeme ya Msongo wa Kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma imekamilika hatua itakayowezesha umeme unaozalishwa katika Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP) kufika Dodoma kupitia Chalinze.

Mramba ameyasema hayo leo, Agosti 18, 2026, wakati akikagua hatua za mwisho za utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Njia ya Kusafirisha Umeme ya Chalinze–Dodoma yenye urefu wa kilomita 345, pamoja na upanuzi wa Vituo vya Kupoza na Kusambaza Umeme vya Chalinze mkoani Pwani na Zuzu jijini Dodoma.

Amesema ujenzi wa njia hiyo umefikia asilimia 99, huku upanuzi wa Kituo cha Zuzu ukiwa umefikia asilimia 98 na kwamba wataalamu wamekamilisha maandalizi ya kuanza kuwasha njia hiyo.
“Kituo cha Zuzu kipo tayari katika hatua za mwisho kabisa. Wataalamu wamenieleza waatanza kuwasha kwa majaribio katika kituo. Umeme utaanza kufika Dodoma kutoka Bwawa la Julius Nyerere kupitia Chalinze hadi kufika Dodoma,” amesema Mramba.

Amesema kukamilika kwa njia hiyo ya kV 400 ni hatua muhimu katika kuimarisha mfumo wa usafirishaji wa umeme nchini, kwa kuwa itapokea umeme unaozalishwa katika Bwawa la Julius Nyerere na kuusafirisha kutoka Chalinze hadi Dodoma, ambako utaingizwa kwenye Gridi ya Taifa na kusambazwa kwenda maeneo mbalimbali nchini.

Aidha, Mramba amesema wanufaika wakubwa wa mradi huo ni Reli ya SGR, akifafanua kuwa njia ya umeme inayotumika kwa ajili ya SGR ilikuwa ikitumika pia kwa matumizi ya watumiaji wengine ambapo kukamilika kwa njia hiyo kutawezesha watumiaji wengine kuondolewa kwenye njia inayotumiwa na SGR, hivyo reli hiyo kuwa na njia yake ya umeme kwa matumizi yake.
Aidha, Mramba amesema utatuzi wa changamoto kama iliyotokea hivi karibuni ya kuzimika kwa Gridi ya Taifa ni kukamilika kwa Njia ya Kusafirisha Umeme ya Chalinze hadi Dodoma, ambayo itawezesha kuwepo kwa utulivu na kuimarisha ubora wa umeme katika Gridi ya Taifa kwa kuwepo kwa umeme wa kutosha.

Amesema kwa sasa mradi huo ni miongoni mwa miradi muhimu kwa nchi, ambapo unagharamiwa na Serikali ya Tanzania kwa asilimia 100 kwa takribani Shilingi bilioni 600, ukiwa ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kusafirisha umeme inayotekelezwa nchini.
Mramba ameeleza kuwa maeneo yatakayonufaika na njia hiyo ya umeme ni pamoja na mikoa ya Kanda ya Ziwa, ikiwemo Mwanza, Shinyanga, Tabora na Kigoma, pamoja na Singida upande wa magharibi. upande wa kaskazini, mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro itanufaika na umeme utakaosafirishwa kupitia njia hiyo.

Mramba amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha utekelezaji wa mradi huo pamoja na usimamizi wa Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi akieleza kuwa kukamilika kwake kutaongeza uwezo wa mfumo wa usafirishaji wa umeme nchini na kuimarisha upatikanaji wa huduma ya umeme yenye ubora na uhakika kwa wananchi.