MAANDALIZI YA MADEREVA WA TEKSI MTANDAO NCHINI KUELEKEA AFCON 2027
Madereva wa teksi mtandao nchini wameanza mikakati ya kuhakikisha wanatoa huduma bora na za kuaminika kwa wageni watakaowasili nchini wakati wa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027).
Katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Madereva wa Teksi Mtandao Tanzania (TODA) uliofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa TODA, Fay Mashala, alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya madereva, serikali, mamlaka za udhibiti, na kampuni zinazoendesha mifumo hiyo ili kuweka mazingira mazuri ya kibiashara, usalama, na uboreshaji wa teknolojia na ubora wa huduma.
Kuelekea mashindano hayo makubwa, sekta hiyo inatarajiwa kuwa na mchango mkubwa katika kuwasafirisha wageni, watalii, mashabiki, na wananchi kote nchini.
Madereva wameaswa kutambua kuwa ndio kioo cha kwanza cha taifa kwa wageni wanaowasili, hivyo wanatakiwa kuhakikisha magari yao yako katika hali nzuri, wanazingatia sheria za usalama barabarani, na wanatoa huduma kwa lugha ya staha na heshima.
Aidha, wamehimizwa kuwa waaminifu kwa abiria na kuepuka tabia ya kuwaomba malipo ya ziada yasiyoainishwa kwenye mfumo wa huduma.
Kwa upande mwingine, serikali kupitia Wizara ya Uchukuzi na Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), imesisitiza kuendeleza ushirikiano na wadau hao ili kuweka mazingira yatakayowezesha usafiri wa kidijitali kutoa huduma zilizo salama na zenye ufanisi mkubwa kwa wananchi na wageni watakaofika nchini wakati wa AFCON 2027.




