CHUO Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimebuni saruji mbadala, ambayo inamuwezesha mjenzi kupunguza gharama.
Akizungumza katika Maonyesho ya Kitaifa ya Ubunifu, Sayansi na Teknolojia, Mhadhiri wa UDSM Kampasi ya Duce, Dk. Aldo Kitalike, amesema saruji hiyo inaweza kutengeneza vifaa mbalimbali ikiwemo matofali, mable na barabara hususani za vijijini.
“Saruji hii inatengenezwa kwa kutumia mabaki ya mimea ya mazao na mabaki ya machimbo mbalimbali ya madini kwa maana ya mawe na udongo mbalimbali kutokana na mazingira husika,” amesema.
Amesema teknolojia hiyo ni rafiki wa mazingira kwa sababu wamekuwa wakitumia takataka, ambazo jamii imekuwa haizithamini, ikiwemo mabaki ya migomba na miwa.