Breaking News

SERIKALI KUONGEZA VITUO VYA MAFUNZO YA TEHAMA VIJIJINI KUKUZA UCHUMI WA KIDITALI

Na Neema Mpaka - Serikali kupitia Tume ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) imeitaka Taasisi ya School of Community Network kuongeza juhudi za kuanzisha vituo vya mafunzo ya TEHAMA katika mikoa mbalimbali nchini, hususan vijijini, ili kuwajengea vijana ujuzi wa kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidigitali.

Akizungumza leo Mei 27, 2025 jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa mkutano uliowakutanisha wanachama wa Taasisi hiyo kutoka ndani na nje ya nchi, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya TEHAMA, Dkt. Nkundwe Mwasaga, amesema kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kufikia malengo ya Kitaifa ya kuwa na uchumi wa kidigitali ndani ya miaka kumi ijayo.
“Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, asilimia 33 ya Watanzania ni vijana wenye umri wa miaka 15 hadi 34, ambao wengi wao wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa ajira. Kupitia mkakati wa uchumi wa kidigitali uliopitishwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mwaka jana, vijana wanapaswa kuchangamkia fursa mpya za kiuchumi,” amesema Dkt. Mwasaga.

Ameongeza kuwa vituo hivyo vimekuwa msaada mkubwa katika maandalizi ya kufanikisha malengo ya Taifa na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, huku akitaja ushiriki wa wawakilishi kutoka mataifa mbalimbali ikiwemo Zambia na Nigeria kama mfano wa mafanikio hayo.
Kwa upande wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Dkt. Jabhera Matogoro, amesema kuwa tangu kuanzishwa kwa vituo hivyo mwaka 2024, Wilaya ya Kondoa imeshuhudia maendeleo makubwa katika TEHAMA, ambapo shule tano zimepatiwa vifaa vya kompyuta.

“Kila shule iliyofikiwa imepata kompyuta 20 kwa ajili ya mafunzo, ingawa bado kuna changamoto ya upatikanaji wa mtandao na baadhi ya sera zinazozuia utekelezaji wa majukumu,” amesema Dkt. Matogoro
Aidha Dkt Matogoro ametoa wito kwa mamlaka ya Mawasiliano na wadau wa Mawasiliano kushirikiana kwa pamoja kuhakikisha huduma hizo za mawasiliano zinafikishwa kwa jamii zinazowazunguka.

Nae washiriki wa mkutano, Mwenyekiti wa Tarime Community Network, Bw. Gamisi Nsiko, amesema kuwa wanashirikiana na kampuni ya Vodacom katika kutoa vifaa vya TEHAMA, ambapo shule nne tayari zimenufaika.

“Shule za Sekondari zilizopokea msaada ni Manga, Unyari, Serengeti na shule ya wasichana Songe. Walimu na wanafunzi wametoa shukrani kwa msaada huo,” amesema Bw. Nsiko.
Naye Mwenyekiti wa Kondoa Community Network, Bi. salama Salum, amesisitiza kuwa ushiriki wao katika mkutano huo ni hatua kubwa katika kufanikisha malengo yao, huku akieleza kuwa wamefanikiwa kusaidia shule za sekondari kuondokana na ufaulu wa daraja sifuri.